Advertisement

MILIKI2

AINA ZA NGOZI YA USO NA LOSHENI/MAFUTA YA KUTUMIA


Watu wengi hupata chunusi, vipele, ngozi kukauka na matatizo mengine katika ngozi zao kwa sababu ya kutumia losheni au mafuta ambayo hayaendani na ngozi zao. Hii huweza kusababishwa na ushauri mbaya kutoka kwa wauzaji wasiojua vizuri vipodozi au kwa wanunuaji wenyewe kutojua vizuri vipodozi.


Ukitaka matokeo mazuri kwenye ngozi na mwili wako kwa ujumla hakikisha unazingatia mambo yafuatayo:
  1. Unaitunza ngozi yako vizuri sana kupitia usafishaji mzuri, ulaji mzuri, kuipumzisha, kuepuka jua kali, kunywa maji ya kutosha, unatumia vizuri vipodozi nk
  2. Unatumia vipodozi vinavyoendana na ngozi yako na mahitaji yako
  3. Unatumia vipodozi vilivyo salama na vyenye ubora wa hali ya juu
Kwa upande wa kuchagua vipodozi vinavyoendana na ngozi yako naomba leo tukufafanulie vizuri ili usipate matatizo tena au kudanganywa na muuzaji wa vipodozi asiye na elimu na ujuzi wa kutosha
AINA ZA NGOZI

Kwanza jua vizuri sana aina ya ngozi yako. Jijue kama una Ngozi kavu (Dry Skin), Ngozi ya mafuta (Oily Skin), Ngozi ya Kawaida (Normal Skin) au Ngozi mchanganyiko (Combination Skin).
Unaweza kujua aina ya ngozi yako kwa kuichunguza wakati wa asubuhi baada ya kuamka au baada ya kuoga na kukaa muda kidogo bila kupaka mafuta.
Ngozi kavu hukakamaa, hupauka, huwa na magamba kwa mbali na haitoi mafuta yoyote. Ukijifuta kwa karatasi nyeupe au ukitumia karatasi ya kupimia ngozi hutoka kavu kabisa na haina matone ya mafuta
Ngozi ya mafuta huwa tepetepe na hujaa mafuta hata kama haujapaka chochote, Ukijifuta kwa karatasi nyeupe au ukitumia karatasi ya kupimia ngozi hutoka na matone mengi ya mafuta ambayo yameungana au yapo karibu karibu
Ngozi ya kawaida huwa kati ya kavu na ya mafuta. Yaani haioneshi mafuta mengi na wala sio kavu. Ukijifuta kwa karatasi nyeupe au ukitumia karatasi ya kupimia ngozi hutoka na matone machache ya mafuta ambayo yapo mbalimbali
Ngozi mchanganyiko ni ile ambayo sehemu huwa kavu na sehemu huwa ya mafuta. Yaani eneo la kutokea kwenye paji la uso na kushuka kupitia kwenye pua (T-Zone) huwa ya mafuta na mashavu huwa ngozi kavu. Ukitumia karatasi nyeupe au karatasi ya kupimia ngozi hutoka na mafuta eneo kutokea kwenye paji la uso na kushuka kupitia kwenye pua (T-Zone) na hutoka kavu eneo la mashavu.
LOSHENI/MAFUTA YA KUTUMIA
Hapa ndipo penyewe. Na ukikosea hautapata matokeo unayoyataka, sana sana utapata matatizo na kupoteza muda na pesa zako.
Kwanza kabisa tambua kwamba losheni na mafuta mengi sana hufanya kazi zinazofanana na hata ufanisi wao hufanana, tofauti zao kubwa ni harufu tu na bei. Kwa hiyo cha muhimu kuzingatia ni aina ya ngozi yako na malengo ya hiyo losheni au mafuta yako.
Tuna mafuta na losheni aina nyingi sana. Zote huwa na mapambo na matangazo aina mbalimbali, ukiongezea na promosheni na maneno ya wauzaji.
Miluzi mingi hupoteza mbwa, ila wewe sio mbwa na usipotee sasa.
  1. Ngozi ya Kawaida
Ngozi ya kawaida ndiyo ngozi nzuri kuliko zote. Siku zote lenga kuwa na ngozi hii ili maisha yako yawe mazuri na kutunza ngozi yako kuwe rahisi.
Kama una ngozi ya kawaida tumia mafuta au losheni mahsusi kabisa kwa ajili ya ngozi ya kawaida. Huwa zimeandikwa “NORMAL SKIN” au “FOR NORMAL SKIN”.
2.  Ngozi ya Mafuta 
Ngozi ya mafuta ipo katika hatari ya kupatwa na chunusi na kusumbuliwa na vumbi na vijidudu. Haihitaji sana mafuta, ila cha msingi ni kuhakikisha haipotezi maji na hakuna chunusi. Kama una ngozi ya mafuta anza kupunguza mafuta na kuifanya iwe ya kawaida ili maisha yako yawe mazuri na kutunza ngozi yako kuwe rahisi.
Kwa upande wa mafuta/losheni tumia yaliyo mahsusi kabisa kwa ajili ya ngozi ya mafuta. Huwa yameandikwa “OILY SKIN” au “FOR OILY SKIN”.
Ukianza kutafuta mafuta/losheni hizo utakuja kugundua kwamba ni adimu sana. Hii ni kutokana na ukweli kwamba ngozi ya mafuta haihitaji sana mafuta au losheni, na badala yake huhitaji vipodozi vingine kabisa kwa ajili ya kupunguza mafuta na kuifanya iwe ya kawaida.
3.  Ngozi Kavu
Ngozi kavu ipo katika hatari ya kupata magonjwa ya ngozi, kuchanika na kuwahi kuzeeka. Inahitaji sana unyevuunyevu na mafuta kuliko ngozi yoyote. Ngozi kavu ni tatizo, hakikisha unaondokana nayo haraka iwezekanavyo.
Tumia mafuta au losheni ambazo ni mahususi kabisa kwa ajili ya ngozi kavu. Na kama ngozi yako ni kavu sana tumia mafuta au losheni kwa ajili ya ngozi kavu sana.
Tumia mafuta/losheni zilizoandikwa “FOR DRY SKIN” au “DRY SKIN”. Kama ngozi ni kavu sana tumia mafuta/losheni iliyoandikwa “FOR VERY DRY SKIN”.
4.  Ngozi Mchanganyiko
Ngozi hii ni hadimu na haina matatizo sana. Cha msingi ni kupata mafuta/losheni mahususi kwa ajili ya ngozi hii na kuitunza vizuri ili iweze kunawiri.
Endapo mafuta eneo la pua yatakuwa mengi au yanakusumbua sana basi unaweza ukayapunguza kwa kutumia vipodozi vya kupunguza mafuta na kuwa na amani zaidi.
Kwa upande wa mafuta/losheni tumia yaliyoandikwa “FOR COMBINATION SKIN”
Baada ya hapo maisha yako yatakuwa poa kabisa.
MAFUTA/LOSHENI KWA AJILI YA ZAIDI YA AINA MOJA YA NGOZI
Kuna mafuta na losheni ambazo zimetengenezwa kwa ajili ya aina mbalimbali za ngozi. Endapo utaweza kujaribu kwa muda kutazama maendeleo na kuwa na uhakika nayo basi yanaweza kukufaa pia.
Baadhi yao huwa ni kwa ajili ya Ngozi kavu mpaka za kawaida. Haya utakuta yameandikwa “FOR DRY TO NORMAL SKIN” au “FOR DRY AND NORMAL SKIN”
Baadhi yao huwa ni kwa ajili ya ngozi kavu mpaka kavu sana. Haya utakuta yameandikwa “FOR DRY TO VERY DRY SKIN” au “FOR DRY AND VERY DRY SKIN”
Baadhi yao huwa ni kwa ajili ya ngozi mchanganyiko mpaka za kawaida. Haya utakuta yameandikwa “FOR COMBINATION TO NORMAL SKIN” au “FOR COMBINATION AND NORMAL SKIN”ngozi 1
Nina imani sasa utakuwa umeelewa vizuri sana na utaweza kuchagua vizuri mafuta/losheni na kushauri watu

Post a Comment

0 Comments